24 Jun 2022 / 88 views
Giggs aachana na Wales

Aliyekua kocha wa Wales, Ryan Giggs ametangaza kujiuzulu rasmi nafasi ya kukinoa kikosi chataifa hilo, baada ya kusimama kazi hiyo tangu mwezi Novemba 2020 akikabiliwa na kesi ya unyanyasaji wa kijinsia alioufanya nyumbani kwake jijini Manchester.

Mchezaji huyo wa zamani wa Manchester United mwenye umri wa miaka 48 alishutumiwa kumshambulia na kumnyanyasa mpenzi wake wa zamani Kate Greville kati ya mwezi Agosti 2017 na Novemba 2020, lakini Giggs amekanusha tuhuma hizo na kukana mashitaka yote.

Katika taarifa yake, Giggs alisema: "Imekuwa ni heshima na nafasi ya pekee kuisimamia nchi yangu, lakini ni vyema shirkisho la soka la Wales, timu ya wakufunzi na wachezaji kujiandaa kwa ajili ya michuano ya kombe la dunia kwa uhakika, bila kuwaza kuhusu nafasi ya kocha mkuu."

Baada ya kutoa taarifa hiyo, Chama cha Soka cha Wales FAW kimetoa shukrani zake kwa Ryan Giggs kwa muda wake aliokuwa kocha wa timu ya taifa ya wanaume na inaheshimu uamuzi ambao amechukua, kwa manufaa ya soka ya la Wales.

Muda wote ambao Giggs alienguliwa kikosini timu ya Wales ilikua chini kocha msaidizi Robert Page aliyeiongoza Wales kufuzu michuano ya Kombe la Dunia kwa mara ya kwanza baada ya miaka 64 bila Giggs. Page ndiye ataoingoza pia timu hiyo nchini Qatar baada ya Giggs kuamua kujiuzulu.