13 Oct 2021 / 106 views
Ronaldo aweka rekodi ufungaji

Mshambuliaji wa timu ya taifa ya Ureno, Cristiano Ronaldo ameweka rekodi ya kufunga jumla ya hat trick 58 katika maisha yake ya mpira baada ya kutupia kwenye mchezo wa kuwania kufuzu Kombe la Dunia mbele ya Luxembourg.

Kwenye mchezo huo wa kuwania kufuzu Kombe la Dunia ikiwa ni kundi A, ubao wa Uwanja wa Algarve ulisoma Ureno 5-0 Luxembourg na kufanya Ureno kufikisha jumla ya pointi 16 ikiwa nafasi ya pili na vinara wa kundi hilo ni Serbia wenye pointi 17.

Ronaldo alitupia mabao mawili kwa penalti ambapo ilikuwa ni dakika ya 8 na 13 na lile la kukamilisha hat trick ilikuwa ni dakika ya 87 akilipachika kwa kichwa na yale mengine mawili yalitupiwa na Bruno Fernandes dakika ya 17 na Joao Palhinha dakika ya 69. 

Kwenye mchezo huo Ureno walipiga jumla ya mashuti 21 na ni mashuti 11 yalilenga lango huku wapinzani wao wakipiga mashuti matatu pekee na ni mashuti mawili yaliweza kulenga lango ila hayakubadilika kuwa bao.